HABARI

HABARI

HABARI

HABARI

HABARI

HABARI

HABARI

UTAFITI NI NJIA YA UHAKIKA YA KUWEZESHA KUWA NA SHERIA MADHUBUTI NA ZENYE TIJA KWA TAIFA- MANDEPO

 


Katibu Mtendaji Tume ya Kufekebisha Sheria Tanzania Bw. George Nathaniel Mandepo amesema kuwa utafiti ni mbinu  muhimu inayoweza kusaidia Serikali  kuamua kama sheria au iboreshwe au ifutwe ili kuendana na mahitaji halisi ya  Taifa kwa wakati husika. 

Akizungumza katika kipindi cha Morning Trumpet cha Azam Tv kinachorushwa kila siku asubuhi kiliendesha mahojiano  kuhusu maendeleo ya sheria nchini, ambapo Bw. Mandepo alisema kuwa jamii inapobadilika, ni lazima sheria nazo zibadilike kulingana na hali. Mabadiliko hayo uhususha pia matokeo ya tafiti mbalimbali za Sheria zinazofanywa na Serikali  hususan kupitia Tume ya Kurekebisha Sheria Tanzania. 

“Utafiti ndio unaoamua kwamba sheria itungwe, ifutwe au iboreshwe,” alisema Mandepo huku akisisitiza umuhimu wa kuihusisha Tume hiyo katika michakato muhimu ya maboresho ya sheria hapa nchini.

Alieleza kuwa tafiti husaidia kubaini changamoto zilizopo kwenye sekta husika na pia ni mbinu ambayo uhusisha  wananchi wanaweza kuguswa au kuathirika kutokana na uwepo au kukosekana kwa sheria katika mbalimbali sekta kama elimu, afya, usalama barabarani na teknolojia. Utafiti hutoa  mwanga kwa watunga sheria kuchukua hatua sahihi, yenye tija na husishi. 

Kwa mujibu wa Mandepo, baadhi ya sheria zimekuwa zikiboreshwa kutokana na mabadiliko ya kijamii na maendeleo ya sayansi na teknolojia hapa nchini.  

Alitoa mfano wa sheria za mawasiliano na matumizi ya mitandao ambazo zimekuwa zikifanyiwa marekebisho mara kwa mara kutokana na ukuaji wa teknolojia duniani.
Mathalani kwa sasa amesema,kwa maelekezo ya Serukali, Tume  hiyo  inaendelea na kazi ya utafiti wa mifumo ya sheria zinazoratibu matumizi ya Akili Ude (Artificial Intelligence ) na utatifi wa mifumo ya Sheria zinaohusu Biashara ya  Hewa Ukaa. 

Kadhalika, alieleza kuwa, miongoni mwa kazi ambazo Tume hiyo imefanya hivi karibuni ni Tathmini na Mapitio sheria za Michezo ya Kubahatisha, Sheria ya Takwimu, Sheria ya Vyama vya Ushirika, Ulinzi Mashahidi na Watoa Taarifa, Matumizi ya Shisha, Bidhaa za Tumbaku na Sigara za Kielektroniki, Sheria ya Usuluhishi  pamoja na Sheria ya Makampuni na Majina ya Biashara. Pia mapendekezo ya kuboresha Sheria yametolewa kwenye Sheria za Usafirishaji Majini na Ardhini.

Aliainisha kuwa kwenye eneo ya haki jinai, Tume hiyo imepitia na kutoa mapendekezo juu ya maboresho ya sheria kwq kuzingatia matokeo ya Tume ya Rais ya Kuangalia Mifumo ya Haki Jinai (Tume ya Hakijinai). Baadhi ya Sheria zilizotazamwa ni pamoja na Sheria za Mwenendo wa Jinai, Sheria zinazogusa dhamana na Sheria ya Uhujumu Uchumi na Uharifu wa Kupangwa. 

Alisisitiza kuwa, kutokea kuanzishwa kwake, Tume imeweza kufanya Tafiti, Tathmini na mapitio ya Mifumo ya Sheria mbalimbali na kutoa Taarifa zaidi ya 70 zilizowezesha Serikali kuboresha sekta husika kwa kutunga, kufuta au kufanya mabadiliko kwenye sheria nyingi zinazogusa nyanja za haki madai na haki jinai, ajira, mahusiano, kazi,  jamii, siasa, uchumi na maendeleo ikiwemo vivutio vya uwekezaji, mifumo ya utatuzi wa migogoro na kodi. 

Tume hiyo imeendelea kutoa Elimu kwa Umma kuhusu sheria mbalimbali kwa nia ya kuwezesha wadau kufahamu haki na wajibu wao ndani ya sheria zilizopo. 

Aidha, wadau wametakiwa kushiriki katika tafiti, tathmiji na mapitio ya sheria na kutoa maoni yao ili kusaidia kujenga sheria bora zinazolinda haki, usawa na maendeleo ya taifa.

WATUMISHI WA TUME YA KUREKEBISHA SHERIA TANZANIA WAMTUNUKU TUZO KATIBU MTENDAJI WA TASISI HIYO KWA UTENDAJI BORA

 



Watumishi wa Tume ya Kurekebisha Sheria Tanzania wamemtunuku Tuzo maalum Katibu Mtendaji wa taasisi hiyo, Bw. George Mandepo, ya kutambua mchango wake mkubwa katika kuimarisha utendaji kazi, ushirikiano na maendeleo ya watumishi ndani ya Tume hiyo.

Tuzo hiyo ilitolewa na watumishi wakati wa Kikao cha Baraza la 24 la Wafanyakazi lililofanyika katika ukumbi wa mikutano wa Tume ya Utumishi wa Mahakama uliopo mjini Dodoma na kuhudhuriwa na viongozi pamoja na wawakilishi wa watumishi wa taasisi hiyo.

Akizungumza kwa niaba ya watumishi wa Tume hiyo wakati wa kikao hicho ,Mwenyekiti wa TUGHE tawi hilo Bi. Vicky Mbunde alisema Bw. Mandepo ameonyesha uongozi wenye weledi, uwajibikaji na usikivu kwa watumishi, hali iliyochangia kuongezeka kwa morali ya kazi na ufanisi katika utekelezaji wa majukumu ya watumishi wa Tume ya Kurekebisha Sheria.

“Katika kipindi cha uongozi wake, tumeshuhudia mazingira bora ya kazi, ushirikiano mzuri baina ya Menejimenti na Watumishi pamoja na kuongezeka kwa ari ya utendaji ndani ya Taasisi,” alisema Vicky Mbunde.

Watumishi hao walieleza kuwa tuzo hiyo ni ishara ya kuthamini juhudi za Katibu Mtendaji katika kusimamia kwa karibu utekelezaji wa majukumu ya Tume ya Kurekebisha Sheria Tanzania pamoja na kuhamasisha uwajibikaji kwa watumishi.

Kwa upande wake Katibu Mtendaji wa Tume ya Kurekebisha Sheria, Bw. George Mandepo aliwashukuru watumishi kwa heshima hiyo na kueleza kuwa mafanikio ya Tume yanatokana na mshikamano na ushirikiano wa pamoja mahali pa kazi.

“Naipokea tuzo hii kwa unyenyekevu mkubwa. Mafanikio tunayoyaona leo ni matokeo ya kazi ya pamoja ya watumishi wote wa Tume ambao wameendelea kutekeleza majukumu yao kwa weledi na kujituma,” alisema Bw. Mandepo.

Aidha, aliwahimiza watumishi kuendelea kufanya kazi kwa bidii, uadilifu na uzalendo ili kuhakikisha Tume inaendelea kutekeleza majukumu yake ya kurekebisha na kuboresha sheria kwa manufaa ya Taifa.

SERIKALI YARIDHISHWA NA UTEKELEZAJI WA MPANGO NA BAJETI YA 2025/2026 YA LRCT- NAIBU WAZIRI.

 


  • Naibu waziri Wizara ya Katiba na Sheria Mhe. Zainabu Katimba akiongea na watumishi wa Tume ya Kurekebisha Sheria Tanzania kwenye Ukumbi wa mikutano wa Tume ya Utumishi wa  Mahakama ulioko Dodoma wakati wa Baraza la wafanyakazi  la Tume hiyo.

  • Naibu waziri Wizara ya Katiba na Sheria Mhe. Zainabu Katimba amesema Serikali inaridhishwa na utekelezaji wa Mpango na Bajeti ya Tume ya Kurekebisha Sheria Tanzania kwa mwaka wa fedha 2025/2026, ambapo imeendelea kufanya tafiti na mapitio ya sheria mbalimbali pamoja na kutoa elimu ya sheria kwa umma.

    Kauli hiyo ameitoa tarehe 14/05/2026 katika ukumbi wa mikutano wa Tume ya Utumishi wa Mahakama uliopo mjini Dodoma wakati wa kikao cha 24 cha Baraza la wafanyakazi wa Tume hiyo ambapo ameeleza kwamba Tume imefanya mapitio ya sheria muhimu zikiwemo Sheria ya Usuluhishi, Sura ya 15; Sheria ya Bima, Sura ya 394; na Sheria ya Bima za Vyombo vya Moto (Magari) Sura ya 169, kwa lengo la kuhakikisha zinaendana na mahitaji ya sasa ya kijamii na kiuchumi.

    Mhe. Katimba alifafanua kwamba Tume inaendelea na mapitio ya Sheria ya Usalama na Afya Mahali pa Kazi, Sura ya 295, Tathmini ya utekelezaji wa sheria zinazohusu umiliki wa mali na rasilimali asilia pamoja na kufanya tafiti katika maeneo mapya kama matumizi ya Akili Unde (Artificial Intelligence), biashara ya hewa ya ukaa, adhabu ya kifo na kifungo cha maisha, na usajili wa mawakili.

    “Hatua hizi zinaonesha mchango mkubwa wa Tume katika kusaidia Serikali kuwa na sheria zinazoendana na mabadiliko ya teknolojia, uchumi na mahitaji ya wakati” alieleza Mhe. Katimba.

    “Ninapenda kutambua kwa heshima kubwa juhudi zinazoendelea kufanywa na Tume ya Kurekebisha Sheria Tanzania katika kutekeleza majukumu yake ya msingi ya kuishauri Serikali kuhusu maboresho ya sheria mbalimbali kwa ajili ya kuendana na mahitaji ya wakati na maendeleo ya Taifa letu” Aliendelea Kusema.

    Aidha Katika mwaka wa fedha 2025/2026, Tume imewasilisha taarifa tano (5) kwa waziri wa katiba na Sheria ambazo ni Taarifa ya Mapitio ya Sheria ya Takwimu, Sura ya 351 na Taarifa kuhusu Utafiti wa Mfumo wa Sheria Zinazosimamia Vyama vya Ushirika, za Februari,2025; Taarifa ya Mapitio ya Sheria Zinazosimamia Udhibiti wa Matumizi ya Bidhaa za Tumbaku, Shisha na Sigara za Kielektroniki, Taarifa ya Tathimini ya Utekelezaji wa Sheria ya Michezo ya Kubahatisha Nchini, Sura ya 41 na Taarifa ya Utafiti kuhusu Mfumo wa Sheria Zinazosimamia Utatuzi wa Migogoro ya Mikopo katika Benki na Taasisi za Fedha, zote za Julai, 2025.

    Awali akimkaribisha Waziri huyo, Katibu Mtendaji wa Tume ya Kurekebisha Sheria Tanzania Bw. George Mandepo alisema Mkutano huo utakuwa na mada zitakazo wasilishwa kwa lengo kuongeza uelewa wa shughuli za Tume, kukuza ujuzi na uzoefu katika kuimarisha utendaji kazi ambazo ni Mada kuhusu ukamilishwaji wa Mpango Mkakati wa Tume wa miaka mitano 2026/2027 – 2030/2031; Mada kuhusu Elimu ya usimamizi wa Fedha (Financial Literacy); na Mada kuhusu Maana ya Maadili na Umuhimu wa Uadilifu katika Utumishi wa Umma.

    Aidha Bw. Mandepo alieleza kuwa mwaka wa fedha 2025/2026, Tume ya Kurekebisha Sheria Tanzania iliidhinishiwa na Bunge kutumia jumla ya Shilingi bilion 7.45 Kati ya fedha hizo, kiasi cha Shilingi bilion 1.775 ikiwa ni kwa ajili ya Mishahara na kiasi cha Shilingi bilion 5,627 ikiwa ni kwa ajili ya Matumizi Mengineyo.

DC. MUSSA KILAKALA AIOMBA TUME YA KUREKEBISHA SHERIA KUFUNGUA TAWI MOROGORO

 

Mkuu wa wilaya ya Morogoro Mh. Mussa R. Kilakala alipotembelea banda la Tume hiyo katika Maonesho ya kibiashara yaliyoratibiwa na Chemba ya Biashara, Viwanda na Kilimo Tanzania (TCCIA) yanayofanyika katika Uwanja wa Jamhuri mkoani Morogoro Novemba 24, 2025 .

Mkuu wa wilaya ya Morogoro Mh. Mussa R. Kilakala, ameomba Tume ya Kurekebisha Sheria Tanzania, kuweka tawi la ofisi yao Manispaa ya Morogoro ili kusaidia wananchi elimu ya kisheria kuhusu changamoto mbalimbali za kisheria wanazopitia.

Mhe.Kilakala aliyasema hayo Novemba 24, 2025 alipotembelea banda la Tume hiyo katika Maonesho ya kibiashara yaliyoratibiwa na Chemba ya Biashara, Viwanda na Kilimo Tanzania (TCCIA) yanayofanyika katika Uwanja wa Jamhuri mkoani Morogoro.

Akizungumza kueleza kuhusu changamoto za kisheria zinazowakabili wananchi wa Morogoro, Mkuu huyo wa Wilaya alisema kumekua na wimbi kubwa la migogoro ya wakulima na wafugaji ambao usuluhishi wake ni kupatiwa elimu ya kisheria ambapo alieleza wengi wao hawana ufahamu, jambo linalopelekea migogoro hiyo kujirudia rudia.

"Sisi hapa tuna Wafugaji na Wakulima wana migogoro ya kisheria kila siku nadhani Tume mlitakiwa muwe na tawi hapa kutusaidia kuwaelimisha" alisema Mh. Kilakala.

Afisa Sheria kutoka Tume ya Kurekebisha Sheria Tanzania, Bi. Jackline Nungu, alisema licha ya kutokua na tawi mkoani hapo bado wananchi wanayo nafasi ya kutumia kipindi hiki cha maonesho kufika bandani hapo kujifunza kuhusu sheria mbalimbali na kueleza kuwa Tume hushiriki katika kampeni na maonesho mbalimbali ili kutoa elimu ya sheria na msaada wa sheria kwa wananchi.

Aidha Jackline aliongezea kuwa kutokana na kukua kwa teknolojia ya habari na mawasiliano, Tume imekua ikitoa elimu kupitia  vyombo vya Habari kama vile, vituo vya redio, televisheni na Magazeti na kuwafikia wananchi wengi zaidi kwa pamoja.

Aidha alieleza kuwa wananchi pia wanaweza kuwafuatilia kupitia tovuti, na anuani za mitandao ya kijamii ili kuendelea kuchangia na kutoa maoni yao ya mapendekezo ya marekebisho ya sheria mbalimbali.

"Tunazo anuani zetu wananchi pia wanaweza kutufuatilia na kutoa maoni tovuti yetu ni www.lrct.go.tz , na kwa mitandao ya kijamii instagram na facebook ni tumesheria.tanzania"  alimaliza akieleza Jackline.

Tume ya Kurekebisha Sheria Tanzania inashiriki Maonesho ya Kibiashara Mkoani Morogoro kwa ajili ya kutoa elimu ya sheria kwa Umma ambapo Maonesho hayo yalianza Novemba 20, 2025 na kutegemewa kuhitimishwa Novemba 30, 2025.

KATIBU MKUU MASWI AHIMIZA UBUNIFU KAZINI, AFUNGUA MKUTANO WA BARAZA LA WAFANYAKAZI LRCT

 

Katibu Mkuu wa Wizara ya Katiba na Sheria, Eliakimu Maswi  wakati wa hotuba yake aliyoitoa  kwa watumishi wa Tume ya Kurekebisha sheria Tanzania wakati wa Baraza la Wafanyakazi lililofanyika tarehe 19.11.2025 katika ukumbi wa mikutano katika hoteli ya Sanaan iliyopo Dodoma Mjini.

Katibu Mkuu wa Wizara ya Katiba na Sheria, Eliakimu Maswi, amewataka watumishi wa Tume ya kurekebisha Sheria Tanzania   kuongeza ubunifu na kutumia maarifa mapya katika kutekeleza majukumu yao ili kuongeza ufanisi na kuendana na mabadiliko ya kiutendaji ndani ya Serikali.

Maswi alitoa wito huo tarehe 19/11/2025 wakati akifungua Mkutano wa Baraza la Wafanyakazi uliofanyika katika Hoteli ya Sanaan, Jijini Dodoma, Kikao kilichowakutanisha wajumbe wa baraza la wafanyakazi watumishi mbalimbali kutoka ngazi mbalimbali za TUGHE Taifa na Mkoa.

Akizungumza wakati wa ufunguzi huo, Maswi alisema Tume   ina nafasi muhimu katika uimarishaji wa misingi ya utawala bora, hivyo watumishi wanapaswa kuongeza ubunifu katika utatuzi wa changamoto, utafiti , na utoaji wa huduma kwa wananchi.

“Watumishi lazima wabuni mbinu mpya za kufanya kazi, kutumia teknolojia ipasavyo, na kufikiri nje ya mipaka ya kawaida. Ubunifu ndiyo msingi wa kuongeza matokeo na kuboresha huduma kwa wananchi,” alisema Maswi.

Aliongeza kuwa ubunifu si jukumu la idara fulani tu, bali ni wajibu wa kila mtumishi, kuanzia ngazi ya chini hadi ya juu. Alisisitiza kuwa Serikali inategemea mawazo mapya kutoka kwa watumishi wake ili kuharakisha maboresho ya mifumo ya sheria na haki.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Baraza la Wafanyakazi  Bw. George Mandepo alieleza kwamba Tume  kwa mwaka wa fedha 2025/26 imejipanga kufanya utafiti juu ya mfumo wa sheria zinazohusiana na biashara ya jewa ukaa, utafiti  kuhusu mfumo wa sheria zinazoehusiana na teknolojia ya akili unde na mapitio ya sheria ya Bima za magari sura ya 169.

 Aidha, kazi nyingine ni mapitio ya sheria ya bima sura 394 na mapitio ya sheria iliyoanzisha Tume ya kurekebisha sheria Tanzania sura ya 171 alieza Mandepo

Hata hivyo  Bw. Mandepo alisema Tume kwa kushirikiana ofisi ya mwanashria mkuu wa Serikali na Wizara ya Katiba na sheria wameunda kikosi kazi ambacho kinaendelea na uchambuzi wa sheria za kipaumbele na uandaaji wa bajeti kwa ajili ya utekelezaji ili kuhakikisha Dira inafikia malengo tarajiwa.

 

KAMISHNA AWASHAURI WATAFITI WA TUME YA KUREKEBISHA SHERIA KUWAFIKIA WANANCHI WA KAWAIDA

 

Kamishna wa Tume ya Kurekebisha Sheria, Bw. Iddi Mandi wakati wa Baraza la wafanyakazi lililofanyika tarehe 18.11.2025 katika hoteli ya Sanaan Mjini Dodoma 

Kamishna wa Tume ya Kurekebisha Sheria, Bw. Iddi Mandi, ametoa wito kwa wataalamu na watafiti wa tume hiyo kuhakikisha kuwa wanapata maoni ya wananchi wa kawaida wakati wa tafiti wanazozifanya ili kuhakikisha maboresho ya sheria yanayopendekezwa yaweze kuwa na manufaa kwa jamii nzima.

Akizungumza wakati wa wasililisho lake kuhusu utafiti wa Kisheria kwa wajumbe wa Baraza la wafanyakazi la Tume hiyo lilofanyika leo tarehe 18. /11/2025 katika ukumbi wa mikutano wa Hoteli ya Saanan Jijini Dodoma, Bw. Mandi alisema kuwa tafiti nyingi za kisheria zinapoishia kufanywa kwenye Taasisi, Wizara mbalimbali na watu mashuhuri, hupunguza uhalisia wa changamoto zinazowakabili wananchi wengi wanaoishi katika maeneo ya pembezoni na miji.

“Ni muhimu tafiti zetu ziwe za kina na zenye uwakilishi mpana. Tunapaswa kuwafikia wananchi wa kawaida, maana wao ndio wahanga wakuu wa sheria tunazozifanyia marekebisho. Hatutaki sheria zinazobaki kwenye makaratasi bila kuwa na uhalisia kwenye maisha ya watu,” alisema Bw. Mandi.

Amesisitiza kuwa ufanisi wa tume hiyo unategemea uwezo wake wa kuwasikiliza wananchi, kuelewa mahitaji yao, na kuyatumia kama msingi wa mapendekezo ya mabadiliko ya sheria.

Kwa mujibu wa Kamishna Mandi, tafiti za kisheria zinapaswa kuwa chombo cha kuhakikisha haki inatendeka na kwamba sheria zinakidhi mahitaji ya kizazi cha sasa bila kupoteza misingi yake ya kulinda maslahi ya umma.

Bw. Mandi ameitaka timu ya utafiti ya tume hiyo kubuni mbinu shirikishi, ikiwemo kufanya mikutano ya hadhara, kutembelea vijiji na vitongoji, pamoja na kuendesha majadiliano na makundi mbalimbali ya jamii ili kupata maoni mapana kabla ya kuandaa mapendekezo rasmi ya marekebisho ya sheria.

Tume ya Kurekebisha Sheria inaendelea na mchakato wa mapitio ya sheria mbalimbali nchini, ambapo ushiriki wa wananchi umetajwa kuwa nguzo muhimu katika kufanikisha marekebisho yenye tija na yanayotekelezeka.

Kikao cha Baraza la wafanyakazi Tume ya Kurekebiha Sheria Tanzania kilihudhuriwa na wajumbe kutoka idara mbalimbali za tume  hiyo na wageni kutoka Chama cha Wafanyakazi wa Serikali na Afya Tanzania (TUGHE) taifa na Mkoa.

Tume ya Kurekebisha Sheria Tanzania Yakutana na Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali Zanzibar Kujadili Utekelezaji wa Mkataba wa Ushirikiano (MoU)




Tume ya Kurekebisha Sheria Tanzania   na Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali ya Zanzibar wakati wa kikao kazi cha kuimarisha utekelezaji wa mkataba wa makubaliano ya ushirikiano (MoU) kati ya pande hizo mbilli uliofanyika katika ofisi hizo mjini Zanzibar

Katibu Mtendaji Tume ya Kurekebisha Sheria Tanzania ( kushoto) akisisitiza jambo wakati wa Kikao kazi kilichofanyika Zanzibar, pembeni ni Naibu Mwanasheria Mkuu wa Serikali ya Zanzibar Bw. Shaaban Abdalla.
Kikao kinaendelea 













Tume ya Kurekebisha Sheria Tanzania   imekutana na Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali ya Zanzibar katika kikao kazi kilicholenga kuimarisha utekelezaji wa mkataba wa makubaliano ya ushirikiano (MoU) kati ya pande hizo mbili, kwa lengo la kuimarisha ushirikiano  katika mapitio, maboresho, na utafiti wa sheria zinazotekelezwa katika Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Mapinduzi Zanzibar.

Kikao hicho kilichofanyika  Zanzibar na kuhudhuriwa na wajumbe kutoka Tume ya Kurekebisha Sheria Tanzania pamoja na maafisa waandamizi kutoka Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali ya Zanzibar kilijadili  mafanikio yaliyopatikana tangu kutiwa saini kwa makubaliano hayo, pamoja na kuweka mikakati ya pamoja ya utekelezaji wa maeneo ya kipaumbele ya kisheria kwa kipindi kijacho.

Akizungumza katika kikao hicho, Katibu Mtendaji wa Tume ya Kurekebisha Sheria Tanzani George Mandepo, alisema kuwa ushirikiano kati ya Tume na Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali ya Zanzibar ni muhimu katika kuimarisha mfumo wa sheria nchini kwa kuzingatia mahitaji ya pande zote mbili za Muungano.

Kupitia mkataba huu wa makubaliano, tunajenga msingi madhubuti wa kushirikiana katika kufanya tafiti za kisheria, kubadilishana uzoefu, na kuimarisha uwezo wa wataalamu wetu wa sheria kutoka pande zote mbili,alisema.

Aidha Bw. Mandepo alisema kwamba LRCT kwa mwaka wa fedha 2025/26 imejipanga kufanya tafiti mbalimbali ikiwemo utafiti wa mfumo wa sheria zinazosimamia upingaji wa maamuzi ya kiutawala mahakamani,utafiti wa mfumo wa sheria zinazosimamia usajili wa Mawakili Tanzania na utafiti wa mfumo wa sheria unaosimamia biashara ya hewa ukaa.

Bw. Mandepo amefafanua kwamba Tume  kwa sasa inaendelea kufanya mapitio ya sheria ya Bima sura ya 169, mapitio ya sheria ya Bima sura ya 394 na mapitio katika sheria ya afya na usalama mahala pa kazi Sura ya 297.

Hata hivyo alieleza kwamba Tume inafanya tathmini ya utekelezaji wa sheria za mamlaka ya nchi kuhusu umilikimali na maliasili za nchi sura ya 449 pamoja na sheria ya mapitio na majadiliano  kuhusu masharti hasi katika mkataba wa mali asili na maliasilia  sura ya 450.

Eneo lingine ambalo limetajwa kufanyiwa tahmini ni katika utekelezaji wa sheria ya ugaidi sura ya 19 sambamba na utoaji wa elimu ya sheria kwa Umma na uandaaji wa machapisho pamoja na ushiriki wa maonesho mbalimbali hapa nchini alimalizia Katibu Mtendaji.

Kwa upande wake, Naibu Mwanasheria Mkuu Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali ya Zanzibar, Bw. Shaaban Abdalla, alieleza kuwa ushirikiano huo unaongeza tija katika kazi za uhuishaji wa sheria kwa kuhakikisha kwamba mabadiliko ya kisheria yanayoletwa yanazingatia uhalisia wa jamii zote.

Tunaamini kuwa kazi za mapitio ya sheria zinahitaji ushirikiano wa karibu kati ya taasisi zote za kisheria katika Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Ushirikiano huu utasaidia pia kuondoa migongano ya kisheria na kujenga msingi wa sheria zinazotekelezeka kwa haki na usawa,alisema.

Katika kikao hicho, wajumbe walikubaliana pia kuunda kikosi kazi cha pamoja kitakachoratibu utekelezaji wa maeneo ya kipaumbele yaliyobainishwa katika MoU, ikiwemo masuala ya sheria za teknolojia, haki za binadamu, usuluhishi wa migogoro, na sheria za kimataifa zinazogusa pande zote za Muungano.

MoU kati ya Tume ya Kurekebisha Sheria Tanzania na Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali ya Zanzibar ilisainiwa kwa lengo la kuimarisha ushirikiano wa kitaalamu, kubadilishana taarifa, na kujengeana uwezo katika nyanja mbalimbali za kisheria, ikiwa ni sehemu ya juhudi za kuhakikisha maendeleo ya sheria yanaenda sambamba na mabadiliko ya kijamii, kiuchumi na kiteknolojia.

MWISHO