HABARI

HABARI

HABARI

HABARI

HABARI

HABARI

HABARI

» » » TUME YA KUREKEBISHA SHERIA YAKABIDHI TAARIFA ZA MAPITIO YA MFUMO WA SHERIA ZINAZOSIMAMIA MAKOSA DHIDI TAARIFA YA MAPITIO YA MFUMO WA SHERIA ZINAZOSIMAMIA UDHAMINI TANZANIA

 












TUME ya Kurekebisha Sheria Tanzania  imewasilisha taarifa mbili za mapitio ya mfumo wa sheria unaosimamia makosa dhidi ya maadili na taarifa ya mapitio ya mfumo wa sheria unaosimamia  udhamini hapa nchini baada ya kufanyiwa utafiti wa kina.

Ripoti hizo zimekabidhiwa jana tarehe 22.09.2023 kwa Waziri wa Katiba na Sheria Mhe. Dkt. Pindi Chana baada ya kufanya ziara katika ofisi ya Tume hiyo  na kukutana na watumishi kwenye ukumbi wa mikutano uliopo katika majengo ya chuo kikuu cha Dodoma (udom) ambapo alipitishwa na kupokea taarifa hizo.

Akiongea kabla ya kukabidhi taarifa hiyo kwa waziri Mwenyekiti wa Tume hiyo  Jaji Mstaafu January Msofe amesema katika kukamilisha mapitio ya Sheria zinazohusu makosa dhidi ya Maadili Tume ilikusanya maoni ya wadau mbalimbali katika mikoa 18  ikiwemo Dodoma, Singida, Mwanza, Mara, Dar es Salaam, Katavi, Geita, Shinyanga, Pwani, Tanga, Iringa, Mbeya, Arusha, Manyara, Mtwara, Lindi, Tabora, Ruvuma na Kigoma.

Jaji Msofe amesema  waliohojiwa ni pamoja na majaji, mahakimu, waendesha mashtaka, mawakili wa kujitegemea, wapelelezi, maafisa ustawi wa jamii, viongozi wa dini, walimu wa shule za sekondari na msingi, watendaji wa mitaa, na asasi za kiraia zinazotoa msaada wa kisheria.

Aidha Jaji huyo ameeleza kwamba utafiti kuhusu makosa dhidi ya maadili ulibainisha  kwamba makosa haya yanaongezeka siku hadi siku jambao ambalo limekuwa tishio kwa taifa .

“ katika mwaka wa 2021 jumla ya makosa 7,601 ya kubaka na kulawiti yaliripotiwa na mwaka 2022 makosa 8,413 yaliripotiwa. Hata hivyo, kesi zinazofunguliwa mahakamani ni chache kuliko zile zinazotolewa taarifa katika vituo vya polisi, kwa mfano  katika kipindi cha 2021/2022 na 2022/2023 Ofisi ya Taifa ya Mashtaka ilifungua Mahakamani kesi 2980 na 4,294  za makosa dhidi ya maadili yakiwemo ya ukatili, kubaka, kujaribu kubaka, kulawiti na kujaribu kulawiti” alisema Mhe. Jaji Msofe.

Mwenyekiti amemueleza waziri wa katiba kwamba kwa mujibu wa utafiti kuna idadi kubwa ya kesi za makosa ya dhidi maadili  ambayo hayajaripotiwa katika vyombo husika huku akibainisha kwamba , makosa dhidi ya maadili yanayotokea mara kwa mara katika jamii ni ubakaji; ulawiti; utoroshaji wa wasichana na walio na umri wa chini ya miaka 16 na shambulio la aibu.

Akizungumzia taarifa ya mfumo wa sheria unaosimamia udhamini  amesema utafiti umebaini kwamba baadhi ya watuhumiwa wa makosa dhidi ya maadili wanaopewa dhamana huruka dhamana hususan watuhumiwa waliopo katika mikoa ya mipakani, hushiriki katika kuharibu ushahidi kwa kuwatisha mashahidi na kurudia makosa ya aina ile ile waliyoshtakiwa nayo.

Akimalizia hotuba yake jaji Msofe amesema kwamba utafiti huo umebainisha changamoto mbalimbali zikiwemo  malalamiko kuhusu watoto kuchanganywa na watu wazima gerezani na hivyo kujifunza mbinu mbalimbali za uhalifu na kuhatarisha maisha yao; mahakama za watoto kukosa miundombinu rafiki kwa ajili ya kusikiliza kesi za watoto; na uhaba wa maafisa ustawi wa jamii unaosababisha mashauri kuchelewa kuisha mahakamani kutokana na takwa la kisheria la uwepo wa afisa huyo wakati wa kusikiliza kesi za watoto.

Naye Waziri wa Wizara ya Katiba na Sheria  Dkt. Pindi Chana amepongeza Tume ya Kurekebisha Sheria Tanzania kwa jitihada wanazozifanya za kupitia sheria na kuja na mapendekezo ambayo utekelezaji wake huheshimisha nchi ndani na nje .

Amesema utafiti uliofanyika kuhusu sheria zinazosimamia maadili  zitakuwa chachu kwenye kuimarisha utamaduni mila na desturi pamoja na Kukuza uhusiano baina ya mataifa ambapo ameeleza kwamba zitaimarisha amani na usalama katika taifa.

Hata hivyo amezipongeza taasisi za kidini ambazo zimekuwa zikisaidia   kuimarisha maadili ya watanzania na kuahidi kuendelea kushirikiana na vyombo vya dini katika kuimarisha amani.

“naipongeza sana Tume ya Kurekeibisha Sheria kwa namna wanavyojitahidi kutafiti sheria na kuja na mapendekezo muhimu, mapendekezo mnayotuletea yamekuwa chanzo cha utulivu wa taifa na zimesisimua ukuaji wa uchumi hapa nchini” Dkt. Pindi Chana.

Hata hivyo Dkt. Pindi Chana ametoa wito kwa watanzania wote kutofumbia macho pindi waonapo vitendo vya ukiukwaji wa maadili  au uvunjifu wa amani huku akieleza kwamba  Wizara ya Katiba na Sheria imeendeLea kutoa  msaada wa sheria kwa wananchi kupitia kampeni ya Mama Samia legal aid Camping yenye lengo la kuwafanya wananchi kufahamu sheria zinazowazunguka.

Awali akimkaribisha Mwenyekiti wa Tume hiyo  Jaji Griffin Mwakapeje  amesema Tume hiyo imefanikiwa kuandaa ripoti 56 kuhusiana na sheria mbalimbali za hapa nchini huku akibainisha kwamba taasisi hiyo imekuwa ikishirikiana na Taasisi mbalimbali za ndani na nje ya nchi ili kufanikisha majukumu yake kwa ufanisi.

mwisho

 


«
Next
Newer Post
»
Previous
Older Post

No comments:

Tuandikie Maoni yako